Kwa Nini Ninaenda Kanisani Jumamosi
Kwa watu wengi, kwenda kwangu kanisani kila Jumamosi inaonekana kuwa ni tofauti mno na utamaduni wa Wakristo wa Jumapili. Wanashangaa kuwa ninawezaje kuchanganyikiwa kiasi hicho hadi kufikia hatua ya kwenda kanisani katika “siku isiyo sahihi”. Hivyo, kwa nini hasa mimi, sawa na mamilioni ya watu wengine kama mimi, huchagua Jumamosi dhidi ya Jumapili? Hebu tafakari hizi hoja tatu ambazo zinaweza kukushangaza.
Sababu ya Kwanza – Neno la Mungu
Ninaenda kanisani Jumamosi kwa sababu ni siku ya kibiblia na uhudhuriaji kanisani siku ya Jumapili siyo jambo ya kibiblia. Pamoja na kwamba Mungu hukubali ibada kila siku ya juma, aliitenga siku ya saba kama siku maalumu ya pumziko. Siku hiyo inaitwa Sabato na ni Jumamosi. Ilitolewa kwa wanadamu kipindi cha uumbaji, yapata miaka 2,000 kabla Wayahudi hawajatokea (Mwanzo 2:1-3). Yesu alisema “Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu” – si kwa ajili ya Wayahudi peke yao (Marko 2:27).
Wakati wa uumbaji, Mungu alifanya mambo matatu kwa makusudi ili kuifanya siku ya saba kuwa yenye utofauti wa kipekee ukilinganisha na siku zingine sita – alipumzika, aliibariki na kuitakasa Sabato (Mwanzo 2:2,3). Hili ni jambo la muhimu sana.
Kwanza, tunahitaji pumziko baada ya kazi na wakati kwa ajili ya kutafakari. Mungu ametuumba kwa namna hii. Hii ndiyo sababu aliitenga siku hiyo ya saba ya kwanza ya uumbaji ili kutumia muda maalumu kuwa pamoja naye. Pili, Mungu alijaza baraka za kiroho katika siku ya saba ambazo hakuziweka katika siku zingine sita. Mwisho, Mungu aliweka mpaka kuzunguka kipindi hiki cha saa 24 na kuiteua kama siku ambayo inapaswa kuwekwa wakfu kabisa kwa ajili ya kudumisha uhusiano pamoja naye.
Endapo mtu atapitia kila fungu kwenye Biblia linalohusu Sabato atangundua baadhi ya mambo ya kushangaza: watu wote wa Mungu wa Agano la Kale walifurahia mibaraka ya Sabato – kumbuka, kwamba hadi kufikia kwa Ibrahimu hawakuwa Wayahudi (Mwanzo 11:26), Yesu aliiheshimu Sabato kwa kuitunza kila juma (Luka 4:16), wanafunzi wa Yesu waliitunza (Matendo 18:4, 11; 16:13), nayo itatunzwa mbinguni na katika nchi mpya (Isaya 66:22, 23). Biblia inawasilisha mduara usiokatika wa utunzaji wa Sabato tangu wakati wa uumbaji wa mwanadamu hadi kwenye dunia itakayokuwa imefanywa kuwa mpya.
Hivyo basi, kwa nini idadi kubwa ya makanisa ya Kikristo huabudu siku ya Jumapili? Jibu ni “desturi”. Unaona, Biblia kamwe haioneshi kumbukumbu ya Mungu kuibadili Sabato kutoka siku ya saba kwenda siku ya kwanza. Badiliko pekee la sheria ya Mungu lililotajwa katika Maandiko limefanywa na shambulio la ujanja la ndani kwa kanisa (tazama Danieli 7:25).
Badiliko hili lilitokea muda mrefu baada ya kufariki kwa wanafunzi wa Yesu. Hadi karne ya tatu na ya nne, historia imeandika kuwa baadhi ya Wakristo waliadhimisha siku ya ibada ya kipagani ya Jumapili kule Roma na maeneo mengine ambapo kanisa lilikuwa linafanya maridhiano ili kuepuka mateso. Kadiri kanisa lililokuwa Roma lilivyozidi kupata nguvu za kisiasa na kugeuka kuwa Kanisa Katoliki la Roma, liliidhinisha rasmi utunzaji wa Jumapili badala ya Sabato. Leo, hii kanisa hilo linaonesha ukweli huu wa historia kama ushahidi kuwa mamlaka yake na desturi zake ni bora zaidi kuliko Mafundisho ya wazi ya Biblia.
Sababu ya Pili – Upendo
Utunzaji wa Sabato si ushupavu wa sheria. Yesu alisema, “Mkinipenda mtazishika amri zangu” (Yohana 14:15). Kwa kuwa Sabato ni siku ya juma ya ibada Kibiblia kwa mujibu wa amri ya nne, na kamwe haijawahi kubadilishwa na Mungu (bali imebadilishwa tu na mwanadamu), na kwa kuwa Yesu mwenyewe aliitunza Sabato, ninaitunza Sabato kutokana na upendo nilio nao kwake.
Zipo sababu nyingi zinazofanya nimpende na kumtii Yesu. Sababu mbili za msingi ni kuwa Yeye ni Mwumbaji wangu na Mwokozi wangu (Yohana 1:1-3; Tito 2:14). Yesu aliiumba dunia kwa siku sita na akapumzika siku ya saba. Sabato ni ukumbusho rasmi wa Mungu au “ishara kati” yake na watu wake kwamba yeye ni Mwumbaji wetu (Kutoka 31:17). Na kabla ya kurudi kwa Yesu, ujumbe kutoka kwa Mungu unamwita kila mmoja wetu “kumsujudia Yeye aliyeziumba mbingu na nchi, na bahari, na chemchemi za maji” (Ufunuo 14:6, 7). Kila wakati “ninapoikumbuka siku ya Sabato na kuitakasa,” ninamheshimu Muumba wangu kuwa ndiye anayeyashikilia maisha yangu mikononi mwake (Kutoka 20:8-11).
Sio tu kwamba Yesu aliwaumba wanadamu, pia anatukomboa kutoka dhambini. Sabato ni ishara maalumu ya wokovu huu – “ishara kati ya Mimi na wao, wapate kujua ya kuwa mimi, BWANA, ndimi niwatakasaye” (Ezekieli 20:12). Kuacha kazi zetu za kidunia zinazotupatia riziki mara moja kwa juma hutukumbusha kuwa hatuwezi kufanya juhudi zozote ili kuupata wokovu wa milele – ni zawadi ya Mungu na sisi ni tegemezi kwake kwa kila kitu (Waebrania 4:4-10). Kwa sababu kama siwezi kumwamini Mungu kunitunza kwa kunipatia riziki siku moja kwa wiki, ninawezaje kumtumaini Yeye kwa uzima wa milele?
Kila Sabato hunikumbusha juu ya upendo ambao Yesu ametupatia kupitia uumbaji na ukombozi. Kama ambavyo maadhimisho ya siku za ukumbusho yanalenga kukumbusha upya upendo wetu kwa wale walio karibu zaidi na sisi, vivyo hivyo Sabato ya siku ya saba ya juma hutukumbusha juu ya upendo wa Mungu na utegemezi wetu kwake kwa maisha ya ulimwengu huu na ule ujao.
Sababu ya Tatu – Uzoefu
Sababu ya tatu kwa nini mimi ninatunza Sabato ni kwa sababu nimeitikia mwaliko wa Yesu kujaribu na kuona kama Neno lake ni kweli. Mara nyingi Mungu hutualika ili tumjaribu. Mojawapo ya matukio hayo hupatikana katika kitabu cha Malaki 3 ambapo hutupatia jaribio kumpatia moja ya kumi ya mapato yetu. Kwa wanaokubali mwaliko wake, ameahidi kutumwagia baraka.
Sabato pia ina jaribio. Mungu hutualika kumpatia moja ya saba ya muda wetu. Endapo tutaitikia mwaliko huo, ameahidi kutubariki. “Kama ukiita Sabato siku ya furaha … ndipo utakapojifurahisha katika Bwana” (Isaya 58:13,14). Ninapata baraka hizi za Sabato kila juma.
Kupumzika siku ya Sabato hunipatia nguvu mpya ya kimwili, kiakili, kijamii, na kiroho. Huniondolea msongo unaotokana na masumbufu ya maisha. Ninafurahia muda usio na mwingiliano pamoja na familia na marafiki, kitu ambacho huufanya urafiki wetu kuwa hai. Kuabudu pamoja na waumini wenzangu hunitia nguvu. Huwa napata ujuzi na hamasa kwa kujifunza Biblia na mahubiri siku ya Sabato.
Sabato hunipatia sababu ya kuacha kazi zote za kidunia kila juma. Kwa kuwa ni amri ya Mungu, haiachi nafasi yoyote ya maridhiano kwa sababu ya mradi muhimu kazini, au kitu kingine chochote kinachoweza kujitokeza. Hii huzuia pumziko la Sabato lisiwe tu nia njema kwamba siku moja nitapumzika. Ni amri ya Mungu – siulizi maswali – hivyo ninaitunza kwa furaha na kuacha kila kitu kwa ajili ya siku zingine sita kama Mungu alivyosema.
Nimegundua kuwa maneno ya Yesu ni kweli – aliifanya Sabato kwa ajili ya mwanadamu (Marko 2:28). Yaani, Sabato sio kitu fulani ambacho Mungu hutufanyia, bali ni kitu maalum ambacho hukifanya kwa ajili yetu. Katika zama hizi tunazoishi zenye shughuli nyingi, ninahifadhi mibaraka chanya yote ambayo ninaipata kwa sababu Mungu ametupatia Sabato kwa ukarimu.
Ninafahamu kwamba kwenda kwangu kanisani siku ya Jumamosi kunaweza kuonekana kama jambo geni. Lakini sasa unaelewa kuwa ninafanya hivyo kwa sababu nimejitoa kuifuata Biblia, ninampenda Yesu kama Mwumbaji na Mwokozi wangu, na nimegundua baraka za Mungu zilizo katika Sabato. Wewe pia unaweza kufurahia uzoefu huu wenye baraka.
Kama ungependa kujua jinsi gani, au unataka taarifa zaidi, wasiliana tu na G.L.O.W. na watakusaidia. www.glowonline.org (GLOW – Giving Light to Our World – Kuangaza nuru kwa ulimengu wetu.) Unaweza kuwasiliana na Kibidula Mission www.kibidula.org au SLP 17, Mafinga, Iringa, Tanzania www.kujifunzabiblia.com